Search En menu en ClientConnect
Search
Results
Top 5 search results See all results Advanced search
Top searches
Most visited pages

    Akisimama kwenye daraja la watembea kwa miguu juu ya mojawapo ya barabara zenye shughuli nyingi zaidi jijini Nairobi, Ann Masiga anatazama mkondo wa mabasi madogo ya kibinafsi ya abiria wanaosafiri kuelekea nyumbani kwao katika jiji. Hata mita chache juu ya msongamano wa magari, hewa inajaa mafusho ya dizeli na petroli. Masiga anafanya kwa bidii pamoja na serikali ya Kenya ili kurekebisha huduma ya usafiri isiyo na mpangilio na ina hewa mbaya.

    “Usafiri bora, maji na nishati, haya ni mambo makubwa kwa nchi hii,’’ anasema Masiga, afisa wa deni jijini Nairobi kwa Benki ya Uwekezaji ya Ulaya. ‘‘Miundombinu mibaya au mifumo mibaya ya usafiri ni kikwazo kwa kila kitu — kuwapeleka watoto shuleni, kupata kazi, kupata chakula, kuenda hospitalini. Sichoki kuangazia mambo haya kwa sababu kazi yangu ina athari chanya kwa Wakenya wengi wa kawaida.’’

    Mojawapo ya miradi mikubwa ya Masiga katika mwaka 2023 ni mtandao wa mabasi ya usafiri-haraka kwa mji mkubwa.’ Kwa sasa, bila mfumo wowote rasmi wa usafiri , Nairobi hivi punde itakuwa na vituo vya mwisho vya basi vya kisasa, majukwaa ya kupanda na kushukia mabasi kwa urahisi, vituo vya mabasi vyenye mwangaza wa kutosha, vijia vya waenda kwa miguu na waendesha baiskeli, na njia za mabasi maalum kwenye barabara kuu zinazojaa watu wengi. Mradi huu unajumuisha mojawapo ya njia za kwanza za mabasi ya umeme katika Afrika Mashariki. Masiga alikuwa mtu mmoja muhimu mwa wale waliounda timu ya Benki ya Uwekezaji ya Ulaya iliyoandaa mkopo wa Euro milioni 201 kwa ajili ya njia ya umeme. Mkataba huu unajumuisha ruzuku ya Euro milioni 32 kutoka Umoja wa Ulaya.

    “Kwa ukweli tutafanya tofauti kwa mfumo wa huduma ya usafiri wa umma wa Nairobi,’’ anasema Masiga, ambaye kazi yake ya muda mrefu kama mfanyakazi wa umma inatiwa msukumo na mama yake, Elisabeth Semo Masiga, muanzilishi wa elimu ya wanawake nchini Kenya na katibu mkuu wa kwanza mwanamke katika Wizara ya Elimu. ‘‘Itakuwa na athari inayoweza kubadilisha mifumo ya usafiri nchini kote.’’ 

    Kuunganisha tabianchi na uvumbuzi nchini Kenya

    Njia mpya ya mabasi ya umeme ni kipimo cha jinsi mustakabali wa Kenya unavyohusiana kwa karibu na tabianchi na teknolojia bunifu. Ikiongoza katika nishati mbadala, nchi inaongeza uekezaji wake katika teknolojia ya kijani, na vile vile kuhimiza biashara kuwa bunifu na kuwa na radhi kubwa zaidi ya kutafuta fursa na ukuaji katika bara zima. Nchi inaendeleza mipango ya kuongeza usambazaji wa chakula, kusaidia mashamba madogo, kuboresha mauzo ya nje na kujumuisha zaidi watu wasiojiweza katika jamii. Basi ya umeme ni mshipa muhimu sana wa moyo katika mwili wa hii Kenya inayotazama mbele, ambapo wakulima wa mahindi hutembea ndani ya mashamba macho yao yakiwa yamefunzwa kwa programu za simu za kuboresha mavuno. Ambapo wazalishaji wa maembe wanatumia teknolojia ya hali ya juu y kuhifadhi baridi ili kuhifadhi mazao. Na viwanda vya jotoardhi vya hali ya juu vya nchi ni mfano wa mipango ya nishati mbadala unaoigwa kote barani Afrika.

    custom-preview
    Ann Masiga anatarajia maendeeleo makubwa katika mtandao wa usafiri wa mji.

    Hii ni Kenya bunifu iliyopata mshirika katika Benki ya Uwekezaji ya Ulaya. Nairobi ni kitovu cha kikanda cha benki ya EU, na takriban wafanyakazi 30 wanaofanya kazi kwa kitengo chake cha maendeleo cha EIB Global. Kitovu cha Afrika Mashariki kinahudumia nchi za Kenya, Ethiopia, Sudan, Sudani ya Kusini, Uganda, Rwanda, Burundi, Tanzania, Eritrea, Djibouti na Somalia. Benki ya Uwekezaji ya Ulaya imewekeza zaidi ya Euro bilioni 1.5 nchini Kenya tangu katikati ya miaka ya 1970 katika nishati mbadala, upatikanaji wa maji safi, maendeleo ya miji, kujumuishwa kifedha na biashara ndogo. Uundwaji wa kitovu mwaka 2021 na wa EIB Global mwaka 2022 unaongeza kuwepo na athari ya Benki katika ukanda bado zaidi.

    Kazi yangu ina athari chanya kwa Wakenya wengi wa kawaida.
    Ann Masiga

    Afisa wa mikopo kwa Benki ya Uwekezaji ya Ulaya

    ‘Tunaweza kufanya mengi zaidi kwa wakati ujao’

    ‘‘Sina sababu ya kuamini kwamba mustakabali wa nchi hii si mzuri.’’
    XN Iraki

    Profesa katika Chuo cha Nairobi

    Hadithi ya Kenya leo ni mojawapo ya hadithi za jadi ziambatanazo na zile za wakati ujao, ya kilimo cha jadi cha wakulima wadogo ambacho hakikuwa na matrekta au mashine pamoja na teknolojia ya nishati ya kijani iliyoendelea sana na mifumo ya malipo ya simu ya kidigitali, ya wanawake wanaofanya kazi katika majukumu ya familia yanayotii wakati na pia kupata vyeo maarufu katika uongozii na uundaji wa biashara.

    ‘‘Ukizungumza na watu hapa, wanaweza kutokuwa na matumaini, lakini ukiona vile tulivyofanya kwa wakati uliopita nchini humu, unasema kwa mwenyewe, ‘Tunaweza kufanya mengi zaidi katika wakati ujao,’’ anasema XN Iraki, profesa katika Kitivo cha Biashara na Sayansi za Usimamizi kwenye Chuo cha Nairobi.

    Iraki amekulia katika kijiji ambacho hakikuwa na umeme, maji ya bomba, friji au jiko. Baadaye alifundisha nchini Marekani , lakini aliporudi nchini kwake alipata msukumo mkubwa wa kufanya uvumbuzi. ‘‘Sina sababu ya kuamini kwamba mustakabali wa nchi hii si mzuri,’’ anasema.

    custom-preview
    XN Iraki anasema kwamba kuna msukumo mkubwa wa kufanya uvumbuzi nchini Kenya.

    Uvumbuzi kwa Kenya ili kuruka hatua ya kuchafua tabianchi

    Ili kuhakikisha mustakabali mzuri, Hatua na uvumbuzi tabianchi vyote ni muhimu sana, barani Ulaya na kwingineko kote duniani. Lakini Afrika imo ndani ya hatari kubwa ya ongezeko la joto la dunia. Bara hili linahitaji trilioni za dola katika uwekezaji wa kijani–na Kenya inalengaa kuwa kwa msitari wa mbele wa mabadiliko.  

    Kenya iko katika nafasi ya kuruka enzi ya ukuaji ya viwanda vinavyochafua kwa uzito, na kuhamia kwenye jamii endelevu zaidi. Mnamo mwaka 2008, nchi iliunda Mpango wa maendeleo wa Vision 2030, ikiwa na lengo la kutumia nishati mbadala ifikapo 2030. Vyanzo vyenye kujirekebisha tayari vinasambaza zaidi ya 90% ya umeme wa Kenya. Nchi imewekeza vikubwa katika nishati itokayo katika maji na mbuga za jua, lakini hasa katika nishati ya jotoradhi. Shughuli za jotoardhi zinazalisha zaidi ya 40% ya nishati ya Kenya.

    Toka miaka ya 1950, ‘‘Kenya ni muanzilishi wa maendeleo ya jotoardhi barani Afrika,’’ anasema Peketsa Mangi, anayesimama katikati ya shamba lenye majani mengi katika Bonde Kubwa la Kenya lenye manyoya ya mvuke mzito, mweupe unaotoa kelele ukitoka ardhini nyuma yake.

    Hata kama alikulia katika Kenya ya kijiji bila nishati katika nyumba inayoangazwa na taa za moshi, Mangi kwa sasa ni meneja mkuu wa maendeleo ya jotoardhi katika kituo cha Olkariamojawapo ya shughuli za jotoardhi duniani. Kikiwa katika takriban kilomita kaskazini ya Nairobi, kiwanja hiki kinakaa katika Hifadhi ya Taifa ya Hell’s Gate

    Hifadhi hii inajulikana kwa miamba mirefu, korongo, minara ya miamba, chemcheni za asili na mito inayopiga risasi za mvuke kutoka chini ya ardhi. Nishati ya jotoardhi huibuka kupitia misitari mirefu yenye hitilafu iliyo katika ukoko wa dunia ipitiayo katikati mwa Afrika Mashariki na kuleta joto la magma ya sayari karibu zaidi na uso.

    Ikuzungukwa kwa pande zote na mashamba na mashamba ya maua, kiwanda cha jotoardhi cha Olkaria huvuta nishati ya dunia kwa kuchimba elfu nyingi za mita katika ardhi, na kukamata mvuke na kuusafirisha kupitia mabomba ili kuendesha mitambo inayotengeneza umeme. Mabomba makubwa meupe yanabeba maji au moshi katika kiwanda chote cha umeme cha Olkaria kilicho na urefu wa taktiban kilimota 70 za mraba. Mabomba yanakaa juu ya nguzo ili kuruhusu wanyama kupita chini, na yana hata vitanzi vinavyowezesha twiga warefu kutangatanga chini kwa uhuru. Katika nyakati za asubuhi, twiga wanakula kifunguakinywa katika miti iliyo karibu na majengo ya jotoardhi.

    ‘‘Bila nishati ya jotoardhi, ingekuwa vigumu sana kwa nchii hii kukidhi mahitaji yake ya nishati,’’ Mangi anasema.

    Kenya ni muanzilishi wa maendeleo ya jotoardhi baraniAfrika.
    Peketsa Mangi

    Meneja wa jotoardhi kule Olkaria

    ‘‘Bila nishati ya jotoardhi, ingekuwa vigumu sana kwa nchii hii kukidhi mahitaji yake ya nishati.’’

    Peketsa Mangi

    Ufadhili wa nishati jadidifu unaharakisha teknolojia ya kijani ya Kenya

    Kenya itaendelea kupanua nishati yake ya jotoardhi, lakini pia inauzisha nje ujuzi kuhusu umeme na nishati ya kijani kwa nchi zingine barani Afrika. Benki ya Uwekezaji ya Ulaya ni mojawapo ya wakimu wakubwa sana wa shughuli za jotoardhi za Kenya, ambapo iliishafanya uwekezaji mwingi mkubwa tangu miaka ya 1980. Hivi karibuni ilifadhili visima zaidi vya maji na mifumo ya kukusanya moshi kule Olkaria mwaka 2017.

    Benki pia ilisaidia shamba kubwa la upepo barani Afrika katika sehemu ya joto na kavu kaskazini mwa Kenya karibu na Ziwa Turkana. Ilitiwa saini ya mkopo wa Euro milioni 225 kwa shamba hili la upepo mwaka 2014 na kutoa msukumo mkubwa katika ufadhili na imani kwa mradi wa muongo wa mzima. Umoja wa Ulaya ulichangia Euro milioni 25 kwa mradi kutoka EU-Africa Infrastructure Trust Fund. Eneo hili sasa lina zaidi ya mitambo 300 ya upepo na linasambaza umeme wa kutosha kwa zaidi ya nyumba milioni.

    Anna Mwangi, mwanafizikia wa jiografia katika kituo cha Olkaria na mshauri mwenye kazi kwa wanawake vijana katika sekta ya nishati, anaona sekta hii kama njia nzuri kwa wanawake kusonga mbele. Kujumuishwa ni mada kubwa katika jamii na tasnia ya Kenya, anasema, kwani wanawake zaidi kwa sasa wanatetea kutendewa sawa na kazi sawa. Mwangi amefanya kazi karibu ya miaka 15 kwa Kenya Electricity Generating Co., shirika la umeme la serikali. Mitazamo ya kijinsia imebadilika katika wakati huu na bado inaendelea. “Kenya imeongoza si yo tu katika sekta ya nishati,” anasema, “lakini pia katika kuwawezesha wanawake katika nyanja hii na kukumbuka nyenzo za wanawake.”

    Lakini mengi zaidi yanahitaji kufanywa. Wanawake bado wanapaswa kufanya kazi kwa bidii mara 10 zaidi ili kutambuliwa katika tasnia yangu,” Mwangi anasema. “Mimi sasa ni mwanamke mwenye uwezo, lakini ninahitaji kuwa tayari pia kuwawezesha wale ambao wanakuja nyuma yangu, ili tushikane mikono. Hawahitaji kwa ulazima kufuata uwayo wangu, lakini tuko hapa kutengeneza njia. ‘’

    Anna Mwangi anasema tasnia ya nishati mbadala inayokua nchini Kenya ni njia nzuri ya kazi kwa wanawake.

    Uvumbuzi kuleta upatikanaji wa chakula

    Ninajivunia kwa ukweli kuwa sehemu ya athari hii.
    Geoffrey Emungat

    Meneja wa hifadhi baridi huko Tatu

    Kampuni nyingi mpya nchini Kenya ziko zinapitisha sera kwa ajili ya usawa wa kijinsia – na kutambua hitaji la hatua za kijamii na mazingira. Cold Chain, kiwanda cha hali ya juu cha kuhifadhi baridi, ilifunguliwa mnamo Agosti 2023 huko Tatu, takriban kilomita 40 nje ya Nairobi, ina sera ya kisasa ya nishati ya kijani na mpango wa kijamii wa kuwezesha wanawake. Kampuni inawahimiza wanawake kufanya kazi katika sehemu yoyote ya shughuli. Pia inaendeleza kazi kwa sekta zisizojiweza kwa jamii. Kituo kinachometameta kwa usafi kilijengwa kwa vifaa fanisi vya nishati na ndilo jengo la nyumba kubwa baridi la aina yake barani, nje ya Afrika Kusini. Kiwanda hiki kilijengwa ili kukidhi viwango vya Uongozi katika Nishati na Usanifu wa Mazingira, mpango wa kuidhinisha wa kijani unaotumiwa duniani.

    Benki ya Uwekezaji ya Ulaya ilisaini uwekezaji wa kununua hisa wa Euro milioni 15 mwaka 2021 na hazina iliyojenga kiwanda cha Tatu. Hazina, inayoitwa ARCH Cold Chain Solutions East Africa, inajenga operesheni za hifadhi baridhi katika sehemu hii ya bara. Hii hazina ya Afrika Mashariki ilisaidiwa na jengo la uwekezaji linalofadhiliwa na nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya.  Kituo cha Tatu ni kamba la johari kwa hazina ya Afrika Mashariki na mradi bendera wa mpango wa Vision 30 wa Kenya. Operesheni hii pia ni sehemu muhimu ya msukumo wa Kenya wa kusaidia mojawapo ya Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa — kumaliza njaa.

    Katiba ya Kenya inasema kwamba kila mtu ana haki ya kutokuwa na njaa na kuwa na upatikanaji wa chalula kizuri. Katika baadhi ya sehemu za Afrika, zaidi ya 50% ya chakula huharibika kabla ya kuweza kuliwa, kwa sababu ya ukosaji wa friji. Itakapokuwa inafanya kazi kikamilifu, Cold Chain itahifadhi ndizi, tufaha, parachichi, bidhaa za kuku na vitu vingine vinavyoharibika. Italinda mazao kwa ajili ya mikahawa na kusaidia kampuni za dawa, hasa zile zinazohifadhi chanjo za COVID-19.

    Geoffrey Emungat anasema kwamba serikali na sekta ya kibinafsi wanafanya kwa bidii kuondoa hatari za kuhifadhi na kusafirisha chakula nchini Kenya.
    “Wakati mwingine ni vigumu kupata kazi kwenye makampuni, kwa sababu ushindani ni mkubwa sana kwa wanawake kupata nafasi.’’
    Rusbellah Abunya

    Dereva wa Forklift huko Tatu

    ‘‘Ukosefu wa usalama wa chakula unasababisha matatizo mengi katika jamii, na kuna pengo kubwa katika hifadhi ya baridi,’’ anasema Geoffrey Emungat, meneja wa majengo kwenye kituo cha Tatu, akiwa anatembea kwa kuzunguka ghala inayometameta. ‘‘Serikali na sekta ya kibinafsi kwa kweli wanajaribu kufanya kwa bidii kazi ya kuondoa hatari za kuhifadhi na kusafirisha chakula, lakini jengo hili pia linataka kuwa na ushawishi mzuri kwa jamii na tabianchi. Ninajivunia kwa ukweli kuwa sehemu ya athari hii.’’

    Kijadi, mifumo mikubwa ya friji haina sifa bora za mazingira, kwa upande mmoja kwa sababu zinatumia nishati nyingi. Cold Chain inaweka paneli za jua ili kutoa 20% ya umeme wa eneo hilo. Nguvu zake nyingi zinatoka katika viwanda vya jotoardhi na umeme wa maji. Na mfumo wake wa friji unaendeshwa na amonia, ambayo haichangii moja kwa moja kwa ongezeko la joto duniani.

    "Singechulia hili kwa urahisi mtu akisema siwezi kufanya kazi kama hii,” anasema Rusbellah Abunya, dereva wa lori la forklift.

    Katika ghala kubwa la kuhifadhi baridi huko Tatu, Rusbellah Abunya anahamisha bidhaa kwenye rafu zinazokwenda zaidi ya mita tano angani akitumia lori lake la forklift. “Wakati mwingine ni vigumu kupata kazi kwenye makampuni, kwa sababu ushindani ni mkubwa sana kwa wanawake kupata nafasi,’’ anasema akiketi ndani ya lori lake. “Wanawake wa Kenya wana nguvu na wanajitegemea. Singechulia hili kwa urahisi mtu akisema siwezi kufanya kazi kama hii.’’

    Kenya kwa kina

    • Kilimo ndiyo injini inayoongoza ya uchumi
    • Sekta kuu ambazo nchi inataka kuboresha ni usambazaji wa chakula, utengenezaji, nyumba za bei nafuu na huduma za afya
    • Inalenga kutumia 100% nishati mbadalaifikapo mwisho wa muongo
    • Kiongozi katika nishati ya jotoardhi na huduma za kulipana kwa simu
    Kitongoji cha Westlands cha Nairobi

    Uvumbuzi unaohimiza jamii jumuishi

     

    Vert, kampuni ya kusindika maembe iliyo huko Masindi katika Machakos, mwendo wa saa moja kwa gari kutoka Nairobi, ni operesheni inayokua huku ikileta matokeo chanya kwa jamii. Vert ilipokea mkopo kutoka Equity Bank,mkopeshaji ambaye ni mojawapo ya wasaidizi wanaoongoza wa mashamba madogo. Equity Bank ilisaini mkataba wa Euro milioni 25 mwaka 2019 na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya na Euro milioni 25 mnamo mwaka wa 2020. Mikataba hii ilijumuisha ruzuku kutoka Umoja wa Ulaya na ilikuwa sehemu ya Kenya Africulture Value Chain Facility. Mpango huu, unaosaidiwa na Umoja wa Ulaya, unayasaidia makampuni kuwa ya kisasa, kuboresha operesheni za wakulima wadogo, kushawisha jamii jumuishi, na kuwasaidia vijana.  

    Vert inasambaza juisi kutoka wawazalishaji wakubwa kama vile Coca-Cola na inauza aina mbalimbali za matunda yaliyokaushwa. Inashirikiana na zaidi ya mashamba madogo 500, hasa hasa yale ambayo ni ekari chache tu. Ili kuwa kuwa kijani kibichi, inatumia mbegu na maganda ya maembe kutia mafuta katika vyombo vinavyochemsha bya kiwanda, pamoja na paneli za jua ili kupunguza kutegemea umeme wa gridi wa taifa. Kampuni hii inatoa kipaumbele kuajiri wanawake na kufanya kazi pamoja na mashamba yanayoendeshwa na wanawake, kwa sababu moja ya malengo ya wamiliki wake ni kuongeza ujasiriamali wa kike.

    “Kenya inaunda mazingira ambayo ni mazuri kwa wanawake kujihusisha zaidi katika uchumi na kuonyesha kile wanachoweza kufanya,” anasema Maina, mkurugenzi mkuu wa Vert.

    custom-preview
    “Kenya inaunda mazingira ambayo ni mazuri kwa wanawake,” anasema Maina, ambaye kampuni yake yake ya maembe inatoa kipaumbele kwa ajira ya wanawake.

    “Sasa hivi, ni uchumi’

    Jackline Musyoka, ambaye ana digrii katika mikrobiolojia na teknolojia ya biolojia, anafanya kama mchambuzi wa maabara katika Vert. Marafiki zake wengi wanatatizika kupata kazi ikiwa si yo lazima kwa sababu ya kutokuwepo kwa usawa, lakini kama matokeo ya uchumi usiotabirika.

    “Nina matumaini kwamba mambo yatakuwa bora zaidi hatimaye, lakini wengi wetu tunapata wakati mgumu,” Musyoka anasema, akipumzika kutoka kazi yake ya kukagua mapipa makubwa ya rojo za maembe ambayo hivi punde yatatumwa kwa kiwanda cha Coca-Cola. “Sasa hivi, ni uchumi. Inawaletea madhara. Huko nje mambo ni magumu. Kila mtu anapambana.”

    “Nina matumaini kwamba mambo yatakuwa mazuri zaidi.”

    Jackline Musyoka
    Mchambuzi wa maabara katika Vert

    Bima bunifu kwa wakulima wadogo

    Iraki, profesa wa Chuo cha Nairobi, anasema kwamba mustakabali wa kiuchumi wa Kenya utakuwa bora ikiwa Wakenya wanafanya kwa bidii zaidi ili kutatua matatizo kwa kufikiri kwa msingi wa bara na dunia zima.

    “Unapoenda katika nchi nyingine barani Afrika, kama Rwanda au Uganda, anasema,” “unaona jinsi Kenya ilivyo sana mbele ya nchi nyingine.”

    Kampuni moja inayojaribu kukua kwa kuwa bunifu zaidi na kutatua baadhi ya matatizo muhimu katika jamii ni Pula, inayotoa bidhaa za bima kwa mashamba madogo. Wamiliki wa mashamba madogo mara nyingi hawana mfumo wa usaidizi na wanapata matatizo pamoja na mvua isiyotabirika, joto na ukame unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

    “Tunapozungumza kuhusu wakulima wadogo, huwa tunaangalia watu ambao wanalima kwa ajili ya kujikimu ulaji, kupata chakula cha kila siku, na labda kuuza mazao yao ili kuweza kupata kipato cha kutumia kulipa ada za shule au kuendesha siku kwa siku nyumba zao,” anasema Faith Kinuthia, mkurugenzi wa operesheni za shamba katika Pula.

    Katika ziara kwenye mashamba madogo katika Kaunti ya Nakuru, takriban masaa manne katika gari kaskazini mwa Nairobi, Kinutia anabainisha kwamba “bima inasaidia kulinda wakulima hawa dhidi ya hatari nyingi, kama ukosefu wa mvua au wadudu na magonjwa. Ikiwa wadudu wanakuja katika shamba na kuharibu mazao, mkulima anamaliza akiwa hana kitu. Ukizungumza na wakulima hawa, bila shaka watakuambia kwamba wanajionea mabadiliko mengi yanayoletwa na madiliko ya tabianchi.”

    Ukizungumza na wakulima hawa, bila shaka watakuambia kwamba wanajionea mabadiliko mengi yanayoletwa na madiliko ya tabianchi.”

    Faith Kinuthia
    Mkurugenzi wa utendaji wa shambani katika Pula

    Jibu la teknolojia ya hali ya juu kwa mabadiliko ya tabianchi

    Wakulima wadogo nchini Kenya wanawakilisha mojawapo ya sehemu kubwa zaidi za wafanyakazi. Na kilimo ni chanzo kinachoongoza cha shughuli za kiuchumi, ajira na uchuuzi wa nje. Kilimo kinaajiri zaidi ya 40% ya wananchi, ikiwemo wananchi wa vijijini, na unaunda zaidi ya 30% ya pato la taifa la Kenya. 

    Pula huwasaidia sehemu ya wananchi hawa kwa hitaji kubwa zaidi kwa:

    • kutumia teknolojia kuchunguza uharibifu kwa haraka
    • ikitoa zana za kidijitali na huduma za ushauri wa kilomo ili kuboresha mazoezi ya kilimo
    • kwa kutumia programu za simu zinazorahishia zaidi maajenti wa shamba wanaofanya kazi kwa karibu na wakulima.  

    Huduma hizi ni muhimu kwani mabadiliko ya tabianchi yanafanya maisha ya wakulima kuwa tete zaidi. 

    Teresiah Wambui, kushoto, na mama yake, Lucy, anasubiri wakati maajenti wa shamba wa Pula wanapima uzalishaji wa shamba lao la mahindi na kuona ikiwa wanastahili kulipwa bima.

    Bima ya tabianchi

    Dominick Wanyoike anaendesha shamba dogo la mahindi katika Kaunti ya Nakuru, eneo linalojumuisha kwa ukubwa wakulima wadogo wanaoishi katika chini ya hekta 5 kila mmoja. Vigezo vya hali ya hewa vinabadilika nchini Kenya, na hili hasa linaumiza sana mashamba madogo, anasema Wanyoike, anayetumia mikono yakemi tupu kutenganisha nafaka kutoka kwa maganda madogo ya mahindi kwenye bustani mbele ya nyumba yake. 

    “Tuliamua kupata bima baada ya mwaka mmoja wa hivi karibuni tulipokuwa tunatarajia mvua kunyesha kama kawaida lakini hazikuja kamwe,” Wanjoike anasema. “Mavuno halisi yalikuwa machache sana, maisha yetu yalikuwa yakianza kuwa magumu zaidi, na ukame unaoongezeka ulikuwa ukifanya maisha kuwa magumu.”

    “Ukame unaoongezeka ulikuwa ukifanya maisha kuwa magumu.”

    Dominick Wanyoike
    Mkulima katika Kaunti ya Nakuru

    Pula ilianzisha rasmi bidhaa zake za bima kwa wakulima wadogo nchini Kenya mnamo mwaka 2015 na inapanua kwenda katika nchi nyingine katika ukanda. Kampuni inaongeza bima katika gharama za mbegu na mbolea, au inatoa bima kupitia ruzuku za serikali. Hii inapunguza gharama ya bima kwa wakulima. Wakulima hulipwa ikiwa mavuno yao ni chini ya kiwango fulani.

    Pula ilipokea ufadhili kwa kampuni inayofadhili biashara zinazoonyesha matumaini makubwa ya kukua, TLcom’s Africa Fund, ambayo inaangazia kampuni za teknolojia zilizo katika hatua za upanuzi. Benki ya Uwekezaji ya Ulaya ni mwekezaji muhimu katika TLcom. Benki hii ilisaidini uwekezaji wa Euro milioni 10 mnamo 2016, na inawazia uwekezaji mwingine kusaidia zaidi ya biashara mpya za barani Afrika. Uwekezaji huu ni sehemu ya kituo cha Boost Africa kinachofadhiliwa na Tume ya Ulaya.

    “Ni muhimu kwamba tunaendelea kuendeleza uhusiano wa kutegemeana na wakulima wadogo na kuwatunza, kuhakikisha wako katika biashara,” anasema Kinuthia, meneja wa Pula. “Hii itasaidia kubakisha kila mtu katika biashara. Hatimaye, kilimo ni uti wa mgongo nchini Kenya."

    Msaidizi wa shamba katika Akaunti ya Nakuru, takriban saa nne kwa gari kaskazini Nairobi.

    Mabadiliko ya usafiri yanayovutia nchini Kenya

    Mabadiliko ya tabianchi, ambayo yana athari mbaya kwa wakulima, pia ni sababu kubwa katika fikra nyuma ya mradi bendera wa mji — mfumo mpya wa mabasi na njia yake yote ya umeme. 

    Barabara za Nairobi mara nyingi huwa zinajaa na msongamano wa magari huenda polepole sana kwa nyakati za kilele. Kuna mabasi machache ya mji, hakuna tramu au treni za chini ya ardhi, na huduma ya reli iliyozuiwa, kwa hiyo watu wanachukua magari ndogo au mabasi yanayoitwa matatu, au wanatumia magari yao wenyewe kufikia mahali fulani. Kadiri idadi ya wananchi inavyokua, msongamano, nyakati za kusafiri, kelele na uchafuzi wa hewa vinaongezeka, pia.

    “Serikali kiukweli inatazama mbele kuboresha hali ya mabasi,” anasema Joseph Kochalle, injinia wa barabara anayefanya pamoja na Mamlaka ya Usafiri wa Eneo la Mji wa Nairobi “Ni siku ngumu, ngumu kufika nyumbani jijini Nairobi au kupanga safari yako.”

    “Mtandao wa usafiri wa mabasi mapya jijini Naironi utasaidia watu wa jijini, uchumi, uchafuzi na msongamano sana, kwa sababu usafiri ni mtafaruku sasa,” anasema, akiketi katika mkahawa katika Kitongoji cha Westlands katikati jijini Nairobi, mita chache tu kutoka mojawapo ya vituo vya mabasi visivyo rasmi vyenye shughuli nyingi zaidi. “Mfumo mpya pia utatoa msukumo kwa maeneo mengine ya miji mikuu ambayo yanakuja pamoja, kama Mombasa na Kisumu,” 

    Njia tano mpya za mabasi jijini Nairobi zitachukua muda unaosalia wa muongo huu ili kukamilika. Mipango ilianza karibu na mwaka 2014, kwa hiyo wakaazi na maafisa wa usafiri wana hamu ya kuharakisha ujenzi. Kenya inatumai mfumo mpya wa kisasa na njia ya umeme itakuwa mfano wa Afrika kwa usafiri fanisi wa kijani.

    ‘Hatua kubwa ya kusaidia maisha yangu’

    Jioni moja katikati jijini Nairobi, Carolyne Omondi anasimama kwa hadhari kando ya barabara kuu yenye shughuli nyingi, akisubiri kuanza safari yake ndefu kuelekea nyumbani katika makazi yasiyo rasmi ya Kibera baada ya siku iliyojaa kazi. Magari, mikokoteni, malori, na lori za mizigo mizito zinapita karibu na miguu yake, akitafuta basi. Kama waenda kwa mguu wengi, Omondi anasubiri katika foleni ndefu na hali zisizo salama ili kupata usafiri kwenye matatu, kwa mara nyingi ambayo ni ya zamani, yenye misukosuko na isiyo na raha.

    Carolyne Omondi, akisubiri kuchukua basi kuelekea makazi yasiyo rasmi ya Kibera jijini Nairobi, anasema si yo rahisi kufika nyumbani baada ya kazi.

    “Siyo uzoefu mzuri, hasa ninaporudi kutoka kazini,” anasema Omondi, msaidizi wa mganga wa meno katikati mwa jiji la Naironi, ambaye anaishi huko Olympic Estate, sehemu ya Kibera ambayo iko katika kilomita tisa tu mbali lakini inachukua angalau saa moja kufika kupitia msongamano wa magari na foleni ndefu za mabasi. “Unachoka na unapaswa kupambana ili kupata basi,” anasema. “Watu ni wagomvi sana, usalama si yo bora, kuna wanyakuzi wa mfukoni.”

    Omondi anataka angetumia muda mfupi zaidi kusafiri. Ingempa muda zaidi wa kupumzika ili kutekeleza lengo lake la kurudi shuleni ili kuwa daktari wa meno.

    “Mabasi na usafiri bora,” anasema, “vingekuwa hatua kubwa ya kusaidia maisha yangu.”